MWENYEKITI wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Balozi Ali Idi Siwa, amesema Mfuko utaendelea kusimamia maono ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuhakikisha Watanzania waliopo kwenye sekta binafsi na sekta isiyo rasmi wanasajiliwa na NSSF pamoja na waajiri kuwasilisha michango stahiki ya wafanyakazi wao.
Balozi Siwa amesema hayo jijini Mwanza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 49 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa NSSF, ambapo aliwataka watumishi wa Mfuko kuendelea kutoa huduma bora, kujielekeza katika matumizi ya TEHAMA, kushirikiana sehemu za kazi na kuifika sekta isiyo rasmi kwani imebeba sehemu kubwa ya Watanzania ambapo kupitia kundi hilo Mfuko utapata wanachama wengi wapya.
Amesema mpango wa mwaka na bajeti pendekezwa ya Mfuko kwa mwaka wa fedha 2022/23, Mfuko umeweka malengo mbalimbali ikiwemo kusajili wanachama wapya 313,478, kukusanya michango ya shilingi trilioni 1.61 pamoja na kukusanya shilingi bilioni 383.5 ambazo ni mapato yatokanayo na uwekezaji.
Amewataka wajumbe wa baraza hilo wakawe kioo kwa wenzao ili Mfuko uweze kuwa na matokeo chanya kwa wanachama na Mfuko kwa ujumla.
Naye, Ibrahim Maftah ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, alisema Mfuko umefanya vizuri katika kutekeleza majukumu yake ambayo ni kuandikisha wanachama, ukusanyaji wa michango, kuwekeza na kulipa mafao.
Amesema Mfuko umefanya mapitio ya Mpango wa Uchangiaji wa Hiari ili kuvutia wanachama wapya kutoka katika makundi mbalimbali ya sekta isiyo rasmi ikijumuisha wakulima, wavuvi, wamachinga, mama lishe, waendesha boda boda na bajaji.
“Lengo la mapitio hayo ni kuongeza wigo wa wanachama na kuwa na mafao yanayokidhi mahitaji ya makundi hayo,” alisema Maftah.
Maftah amesema katika mwaka wa fedha wa 2022/23, Mfuko unategemea ongezeko la wastaafu 30,084 kutoka wastaafu 20,894 mwishoni mwa mwaka 2021/2022.
Awali, Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu na Utawala, Ekwabi Mujungu, alisema watumishi wako tayari kuendelea kutoa huduma kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
Kwa upande wake, Willy Kibona ambaye ni Mkuu wa Sekta ya Fedha TUICO Taifa amesema kazi kubwa ya baraza hilo ni kuishauri Menejimenti kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo kupitia mpango wa mwaka na bajeti ya Mfuko kwa mwaka wa fedha 2022/23 pamoja na makadirio ya mapato na matumizi.
“Tunashukuru kwa somo tosha kutoka kwa mgeni rasmi ambalo litaweza kusaidia kujadili kushauri na hatimaye yale yatakayokuwa tumependekeza tutakapokuja kwako kwenye Bodi yapate baraka,” alisema Kibona.
Na MWANDISHI WETU
Matukio katika picha wakati wa Kikao cha 49 cha Baraza kuu la wafanyakazi wa NSSF kilichofanyika jijini Mwanza






