KATIBU Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Baishara, Doto James, amekutana na Wakurugenzi Watendaji kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Francis Nanai, na Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Biashara Dkt. Godwill Wanga, katika ofisi za banda la Tanzania kwenye maonesho ya Expo 2020 Dubai.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Balozi Mohammed Mtonga, Kamishna Jenerali wa Maonesho ya Expo 2020 Dubai na Balozi wa Tanzania Umoja wa Falme za Kiarabu, Balozi Shaban Baraza, Balozi Mdogo UAE, Dubai na Mkurugenzi wa Banda la Tanzania kwenye Maonesho ya Expo 2020 Dubai, Getrude Ng’weshemi, kutoka TanTrade ambao ni waratibu wa Maonesho hayo ya Kimataifa yanayoijumuisha Tanzania kati ya nchi 191 Duniani zinazoshiriki katika maonesho hayo.
Lengo la kikao hicho ni kuangalia kwa namna gani Sekta Binafsi zinashiriki kikamilifu na kuchochea msukumo wa ushiriki kwa Watanzania kwa ujumla katika monesho hayo ya Expo 2020 Dubai yanayofanyika kwa muda wa miezi sita.
Katika kikao hicho Katibu Mkuu pamoja na mambo mengine amesisitiza ushiriki wa Tanzania hasa Sekta Binafsi katika uratibu na uendeshaji wa programu mbalimbali katika Maonesho hayo ili Tanzania iweze kutumia fursa ya maonesho hayo kwa lengo la kuvutia uwekezaji.
Aidha, TanTrade ikiwa ndio mratibu wa Maonesho hayo, tayari wameshaanda
utaratibu maalum kwa ajili ya ushiriki wa Sekta Binafsi, hivyo ni muhimu kuwasilisha fursa zinazohitaji wawekezaji ili kuratibu mikutano ya kibiashara baina ya wadau wa Sekta Binafsi na Wawekezaji mbalimbali.